Katibu wa 
Sekretarieti ya Ajira katika Utumishi wa Umma anapenda kuwataarifu 
waombaji kazi waliofanya usaili wa mchujo kwa nafasi mbalimbali za 
Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) kuwa matokeo ya usaili huo yanatarajiwa kutolewa katika kipindi kisichozidi siku kumi (10) kuanzia siku ya tangazo hili.
Amesema kuwa 
kutokana na muitikio mkubwa wa waombaji kazi waliojitokeza kwenye usaili
 huo, kwa sasa zoezi linaloendelea ni kusahihisha mitihani hiyo ambayo 
inatarajiwa kukamilika ndani ya muda huo. Ratiba kamili ya usaili wa ana
 kwa ana (oral Interview) kwa kila kada itatolewa pamoja na majina ya 
waliofaulu usaili wa mchujo.
Aidha, 
amesisitiza waombaji kazi wote waliofanya usaili huo kuendelea kujiandaa
 kwa ajili ya usaili unaofuata kwa wale watakaochaguliwa, ili kujiweka 
katika nafasi ya kufanya vizuri kutokana na ujuzi na weledi walionao 
katika taaluma zao na hatimae kuwa miongoni mwa watakaofanikiwa 
kuajiriwa katika Utumishi wa Umma kupitia mamlaka hiyo.
Amewataka 
wasailiwa watakaoitwa kwenye usaili wa mahojiano watatakiwa kuja na 
vyeti vyao halisi kuanzia cheti cha kuzaliwa, cheti cha kidato cha nne, 
kidato cha sita, Astashahada, Stashahada ya juu, Shahada na kuendelea 
kulingana na kiwango cha elimu waliyonayo. Aidha kwa wale waliosoma nje 
ya Nchi wafike na cheti cha uhakiki toka Mamlaka zenye dhamana ambazo ni
 TCU, NACTE na NECTA.
Sambamba na hayo,
 anawakumbusha wasailiwa hao kuendelea kutunza namba zao za usaili kwa 
kuwa matokeo yote yatatolewa kupitia namba walizopewa wakati wa usaili.
Usaili huo wa 
mchujo ulifanyika kwa muda wa siku tatu  katika kanda kumi ambazo ni 
Zanzibar, Mbeya, Dodoma,  Arusha, Mwanza, Morogoro, Mtwara, Tabora, 
Iringa na Dar es Salaam kulikokuwa na vituo viwili vya usaili ambavyo ni
 Chuo cha Kikuu Kishiriki cha Elimu (DUCE) na  Chuo cha Kumbukumbu ya  
Mwalimu Nyerere, Kigamboni.
 Imetolewa na Kitengo cha Mawasiliano Serikalini, Sekretarieti ya Ajira katika Utumishi wa Umma tarehe 6 Septemba, 2017.
TANGAZO KWA WAOMBAJI KAZI WALIOFANYA USAILI WA NAFASI ZA TRA.
 
        Reviewed by ISSAH JUMA
        on 
        
Tuesday, September 12, 2017
 
        Rating: 
      
No comments: